Mwanachuoni mtajika wa Iran marhum Ayatullah Mohammad Reyshahri, katika kitabu kiitwacho "Seerah ya Mtume wa Mwisho", anaashiria sifa zake kuu. Katika makala hii tunaangazia misingi muhimu sita amayo Mtume Muhammad SAW alishikamana nayo katika maisha yake yote.
Msingi wa kwanza ni kwamba mienendo yote ya Mtume Muhammad SAW inaafikiana na akili. Hapa, akili haimaanishi akili kama wengi wanavyoielewa bali inarejelea uwezo wa kumlinda mtu kutokana na vitendo visivyofaa. Imam Sadiq (AS) anasema kwamba Mwenyezi Mungu hakutuma mjumbe isipokuwa akili yake ilikuwa kamilifu. Tukangazia nafasi ya akili katika maisha ya Mtume, tunaweza kusema kwamba matendo yake yote yamewiana na uchambuzi wa kimantiki.
Msingi wa pili ni kushikamana na kuheshimu haki. Kimsingi, Qur'ani Tukufu imejipa sifa kadhaa na pia imeupa sifa bora ujumbe wa Mtume SAW. Moja ya sifa hizi ni “sidq” (mkweli) na jingine ni “haqq” (haki). Kwa hiyo, hakuna shaka kwamba mwenendo wa maisha ya Mtume SAW uliegemezwa kwenye haki. Hapa haki inahusu jambo linaloeleweka ambalo ni sahihi. Kwa kweli, kile kinachobaki kuwa kweli na kisichobadilika baada ya muda kinakuwa haki. Tabia ya Mtume Muhammad SAW pia ilikuwa sahihi na thabiti.
Msingi wa tatu ni kukuza haki. Anarejelea Aya ya Qur'ani Tukufu na kusema, Nimeamrishwa nikufanyieni uadilifu. Katika sehemu nyingine, anasema kwamba mtu anakuwa mwenye haki iwapo anapenda watu wapate kile anachopenda yeye mwenyewe.
Msingi wa nne ni kuwa mkarimu. Hapa ukarimu ni pamoja na mambo mengi kama vile kuwalisha na kuwavisha wengine, kusaidia wengine kifedha, nk.
Matendo ya Mtume SAW pia yalikuwa mazuri, na kwa mfano, kama angetumia panga, alikuwa na umahiri mkubwa. Imam Ali AS anasema kwamba mtu aliyepigana bega kwa bega pamoja na Mtume anachukuliwa kuwa jasiri katika vita.
Msingi wa Tano ni kuwa, hakujitenga na jamii. Alikula chakula sawa na watu wengine. Kwa mfano hata mavazi yake yalikuwa ya kawaida kiasi kwamba ilikuwa vigumu kwa wageni wa Madina kumtofautisha na masahaba zake.
Msingi wa sita ni unyenyekevu. Hapa unyenyekevu unamaanisha kuwa na maisha ya kawaida bila gharama kubwa. Hakupendezwa na vitu vya kistarehe na bei ya juu. Alikuwa akiongea na kucheza na watoto na kuwakaribisha kibinafsi wageni. Zote hizi ni dalili kuwa Mtume Muhammad SAW aliishi maisha ya kawaida na hivyo amekuwa ni kigezo cha kuigwa na ruwaza njema.