Shirika Rasmi la Habari la Syria, SANA limeripoti kuwa, basi moja la abiria lililokuwa likipita katika barabara ya Deir ez-Zor kuelekea Tadmir katikati mwa Syria lilishambuliwa na magaidi wa kundi la Daesh na kusababisha vifo vya watu wasiopungua 25 na kujeruhiwa wengine wanane. Baadhi ya duru zinasema idadi ya waliofariki imeongezeka na kufika 28.
Picha zilizorushwa kutoka eneo la tukio zinaonyesha namna basi hilo la abiria lilivyoteketea kikamilifu. Baadhi ya maeneo ya misituni katikati mwa Syria baadhi ya wakati hukumbwa na mashambulizi ya masalia ya kundi la magaidi wakufurishaji la Daesh au ISIS.
Bado kuna masalia ya wanachama wa kundi la kigaidi la Daesh katika maeneo ya msituni katikati mwa Syria licha ya kundi hilo la kigaidi kusambaratishwa nchini humo. Masalia hayo hutekeleza mashambulizi ya kiholela katika maeneo mbalimbali nchini humo.
Mgogoro ulianza huko Syria tangu mwaka 2011 kufuatia hujuma kubwa ya makundi mbalimbali ya kigaidi kwa uungaji mkono wa Saudi Arabia, Marekani na nchi kadhaa nyingine kwa ajili ya kubadili mlingano wa kieneo kwa maslahi ya utawala wa Kizayuni. Jeshi la Syria hivi karibuni lilifanikiwa kufunga faili la kundi la kigaidi la Daesh huko Syria kwa msaada wa washauri wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Russia.