IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Pendekezo la Marekani la Mazungumzo ni hadaa, lengo ni kutaka kuipokonya Iran silaha na uwezo

18:26 - June 26, 2019
Habari ID: 3472018
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa lengo kuu la pendekezo la Marekani la kufanya mazungumzo na Iran ni kutaka kulipokonya taifa la Iran silaha na sababu za nguvu na uwezo wake.

Ayatullah Ali Khamenei ameyasema hayo leo Jumatano mjini Tehran katika hadhara ya majaji na maafisa wa Idara ya Vyombo vya Mahakama hapa nchini. Ameongeza kuwa, pendekezo la mazungumzo la Marekani ni hadaa, na Wamarekani ambao wamepatwa na wahka na woga kutokana na uwezo wa taifa la Iran, wanaogopa kusonga mbele; kwa msingi huo wanataka kuipokonya Iran silaha hizo na sababu za uwezo wake. 

Ayatullah Khamenei ameashiria tuhuma, kejeli na matusi yanayotolewa na utawala mshari zaidi dunia yaani Mrekani dhidi ya taifa la Iran na kusema: Utawala unaochukiwa zaidi na habithi zaidi duniani ambao ndio unaosababisha vita, mifarakano na kupora mali za nchi na mataifa mbalimbali, umekuwa ukilitusi na kutoa tuhuma dhidi ya taifa sharifu la Iran kila siku lakini Wairani hawashtushwi na matendo hayo maovu ya Marekani na wala hawatarudi nyuma. 

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa vikwazo vya Marekani ni dhulma kubwa kwa taifa la Iran na kuongeza kuwa: Muoanisho wa utambulisho wa Kiirani na sifa za Uislamu hapa nchini katika kipindi cha miongo minne iliyopita umebatilisha mashinikizo ya mabeberu wa dunia na kuyafanya yasiwe na taathira yoyote katika harakati ya taifa la Iran.

Ayatullah Ali Khamenei amesisitiza kuwa, kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu, taifa lililodhulumiwa lakini imara na lenye nguvu la Iran litaendelea kusimama kidete kama mlima na kudumisha harakati yake kwa nguvu zote na hatimaye kutimiza malengo yake yote. 

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa mahudhurio makubwa na ya daima ya wananchi katika maandamano ya tarehe 22 Bahman (11 Februari kuadhimisha ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu), maandamano ya Siku ya Kimataifa ya Quds na kushiriki kwao katika chaguzi mbalimbali ni kielelezo cha azma kubwa ya taifa. Ameongeza kuwa, licha ya tashwishi zinazoenezwa na baadhi ya watu, mwishoni mwa mwaka huu wananchi wa Iran watashiriki kwa wingi katika uchaguzi na kuonesha adhama yao. 

Vilevile amezungumzia jinsi Marekani inavyotumia vibaya suala la haki za binadamu na kusema: "Haki za binaadamu ni kuwa wanaaua wasafiri 300 wasio na hatia wakiwa kwenye ndege ya abiria angani na wanaendelea kufanya jinai. Kwa msaada wa Saudia wanaua raia huko Yemen. Raia hao wanauawa wakiwa masokoni, misikitini, matangani na kwenye sherehe na katika mahospitali na kisha wanadai kutetea haki za binadamu!"  

3822447

captcha